Alhamisi, 5 Septemba 2013

Kagame kiburi



                        Kagame kiburi
                                                                             September 1, 2013,


*Wanaompa jeuri sasa waanikwa, yamo mataifa makubwa
*Vyombo vya kimataifa vyatumika kumkingia kifua kila kona
*Uamuzi wa Kenya, Uganda, kujitoa bandari Dar wahusishwa

Na Mwandishi Wetu

RAIS wa Rwanda Paul Kagame bado anaonekana kuwa na kinyongo na Rais Jakaya Kikwete tangu alipopewa ushauri wa kukaa meza moja na waasi ili kumaliza migogoro iliyopo.

Hata hivyo imeelezwa kuwa Rais Kagame anaonekana kuwa na kundi nyuma yake ambalo linampa kiburi na kujiamini kwa kila anachokifanya na ndio maana hakuna mahali ambapo anaonesha kuwa tayari kutumia busara kumaliza tofauti iliyojitokeza.

Tayari Rais Kikwete ameweka wazi kuwa Serikali yake haipo tayari kuingia kwenye malumbano na Rwanda wala nchi nyingine yoyote na kwamba kuhusu Rwanda busara itatumika kutafuta ufumbuzi wake.

Kauli ya Rais Kikwete imekuja baada ya Rais Kagame kutoa kauli za kejeli baada ya kushauriwa na Rais Kikwete kuwa ni vema akakaa na vikundi vya waasi kutafuta ufumbuzi wa kumaliza migogoro nchini Rwanda, ushauri ambao unaonesha kutomfurahisha Kagame.

Wakizungumza wiki hii baadhi ya wachambuzi wa siasa za kimataifa, wameliambia Jambo Leo Jumapili kuwa Rais Kagame anaonekana kuwa na kiburi na hiyo inatokana na kutumia mataifa mengine kuonesha kukasirishwa kwake na ushauri wa Rais Kikwete.


Kwa mujibu wa wachambuzi hao, ni kwamba Rais Kagame anapata kiburi kwasababu pia kuna mataifa makubwa ambayo yanampa msukumo wa kutaka uhusiano wa nchi hizo mbili kuendelea kuwa kwenye kutetereka ingawa Serikali ya Tanzania imezidi kuweka wazi uhuasiano wa nchi hizo si mbaya kama ambavyo inaelezwa.

Kitendo cha Rais wa Rwanda Paul Kagame kutokuwa tayari kuumaliza mgogoro huo, mjadala mkubwa umezidi kuibuka kutokana na kutetereka kwa uhusiano kati ya Tanzania na Rwanda huku Rais wa Paul Kagame akidaiwa kuwa ana kiburi ndio maana hadi sasa hajaonesha kutokuwa tayari kukaa kwenye mazungumo kutafuta muafaka

Wakizungumzia zaidi nguvu ya Rais Kagame, ni kwamba inawezekana pia inatokana  na namna ambavyo anatumia vyombo vya habari vya kimataifa kuelezea uhusiano wake na Tanzania.

Pia nguvu ya wanaomuunga mkono Rais Kagame imedaiwa kuwa ndio inayoendelea kumpa kiburi cha kutokuwa tayari kukaa na vikundi vya waasi kutafuta suluhu.

Wakati hayo yakiendelea duru za kimataifa zinafafanua kuwa Rais Kagame huenda anapata kiburi kutokana na kupewa nguvu na aliyewahi kuwa Rais wa Marekani Bill Clinton.

Siku za hivi karibuni baadhi ya vyombo vya habari vya kimataifa na mitandao ya kijamii vimemnukuu Clinton akitoa kauli za kumkingia kifua Rais Kagame.

Rais Kagame amekuwa akituhumiwa kufadhili kundi la waasi la M23 ambalo lipo kwenye mapigano ya muda mrefu nchini Congo lakini pia Clinton alinukuliwa akimtetea Rais Kagame na kumsafisha dhidi ya tuhuma hizo.

Hata hivyo Rais Kagame mwenyewe amekuwa akikanusha kuhusika kulifadhili kundi hilo kwa namna yoyote ile, na hilo amekuwa alisisitiza mara kwa mara inapotokea mataifa mengi kumtuhumu.

Taarifa zaidi kuhusu Rais Kagame, kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari vya kimataifa, vinadai kuwa mbali ya Clinton kumtetea  pia baadhi ya nchi za Jumuia ya Afrika Mashariki nazo zinaonekana kumuunga mkono harakati zake za kuiendelea kutokuwa na uhusiano mzuri na Tanzania.

Miongoni mwa wanaotajwa kuwa nyuma ya Rais Kagame ni baadhi ya viongozi wa Serikali ya Uganda na hiyo inatokana na kile kinachoelezwa kuwa aliwahi kuwa  Mkuu wa Idara ya Usalama wa Rais Yoweri Museveni wa Uganda kabla ya kujiunga na chama cha RPF.

Ushirika huo wa Kagame kwa Rais Museveni, unatajwa kuwa ndicho kinachotafsiriwa sasa kwamba kinawafanya waendelee kushirikiana.

Pia ilibainishwa kwamba ushirika wa Marekani chini Clinton kwa Kagame, ulikuwa umeshika kasi na hivyo kufanya Taifa hilo kubwa Duniani kukiunga mkono chama cha RPF alimokuwa Kagame.

Kwa mujibu wa taarifa zilizosambaa katika baadhi ya mitandao ya kijamii, jeuri hiyo ya kuwa na vigogo wanaomkingia kifua, ndio inayompa uwezo Kagame kuendelea kuvuruga uhusiano baina ya nchi yake na baadhi ya nchi nyingine ikiwemo Tanzania.

Taarifa zaidi zilidai kuwa hata kitendo cha Rwanda kuamua kujitoa kutumia Bandari ya Dar es Salaan kupitisha mizigo yao ikiwa ni sehemu ya kuonesha hasira zake dhidi ya Tanzania.
Mbali ya Rwanda pia Uganda na Kenya nazo zimejiondoa kutumia bandari hiyo na sasa wamepanga kutumia bandari ya Mombasa.

Kabla ya uamuzi huo wa kujiondoa nchi za Uganda na Rwanda zilikuwa zikitumia bandari ya Dar es Salaam kama kituo cha kupitishia mizigo yao.

Uamuzi wa kutotumia bandari ya Dar es Salaam kwa nchi hizo unaanza leo (Septemba Mosi), unafanyika baada ya mazungumzo ya faragha yaliyomshirikisha Rais Kagame na Rais Museveni na Serikali ya Kenya.

Wakati hayo yakiendelea, Watanzania na Afrika Mashariki imeshuhudia pia wabunge wa Jumuia ya Afrika Mashariki (EALA), wakishindwa kufanya kikao cha Bunge hilo baada ya kutolewa hoja kuwa umefika wakati kwa wabunge wa Bunge hilo kufanya mikutano yao kwa kuzunguka nchi husika.

Hoja hiyo inaonekana ni mwendelezo wa kulipa kisasi dhidi ya Tanzania kwani ukiondoa wabunge wanaowakilisha nchi hii, wabunge kutoka Rwanda, Kenya, Uganda na Burundi wameamua kuunga mkono licha ya kwamba haikuwa sehemu ya ajenda ambayo itajadiliwa kwenye kikao hicho.

Akizungumza kwenye kikao hicho hivi karibuni, Mbunge kutoka nchini Kenya Peter Mathula, aliamua kuwasilisha hoja binafsi akitaka kutenguliwa kwa uamuzi wa vikao vya Bunge hilo kufanyika tu mjini Arusha Tanzania.

Vikao hivyo vimekuwa vikifanyika Arusha nchini Tanzania ambako ndiko makao makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Mbunge huyo alijenga ushawishi kwa wabunge wa Bunge hilo, kukubali vikao hivyo kufanyika kwa mzunguko katika maeneo ya nchi hizo zinazounda Jumuia hiyo.

Hata hivyo kuwasilishwa kwa hoja hizo, kulizua malumbano huku wabunge wa Tanzania wakionekana pekee wakiipinga hoja hiyo.

Mbunge wa EALA kwa upande wa Tanzania Abdullah Mwinyi, aliongoza wabunge wa Tanzania kutoa nje ya ukumbi wa Bunge na kususia kikao hicho.

Hatua ya wabunge wa nchi zote zinazounda Bunge hilo kuwa na umoja wa kupinga vikao hivyo kufanyika Tanzania, imetafsiriwa kuwa ni mwendelezo wa mpango wa kuvuruga umoja uliokuwapo hapo awali.

Hata hivyo, baada ya mvutano huo, kikao cha uongozi wa Bunge hilo, kilifikia makubaliano ya vikao hivyo kufanyika kwa mzunguko.

Bunge la Tanzania kutokana na uhusiano tete kati ya Tanzania na Rwanda, wiki hii limeamua kuomba msimamo wa Serikali ya Tanzania ili kujua namna ambavyo limejipanga kutafuta suluhu.

Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni Freeman Mbowe aliitaka Serikali kuelezea msimamo wake hasa kutokana na kuonekana Rais Kagame hakufurahishwa na ushauri wa Rais Kikwete ambapo Waziri Mkuu Pinda wakati anatoa msimamo alisema Serikali ya Tanzania inaamini busara itatumika kupata ufumbuzi wake.

Pinda alisema Rais Kikwete ameeleza kwa kina kuhusu chanzo cha kutokuwepo kwa uhusiano mzuri na Rwanda , lakini bado alifafanua kuwa tayari Rais Kikwete amemuomba Rais Museveni kusaidia kupata kwa ufumbuzi wa suala hilo.

“Serikali tuaamini kuwa tutamaliza suala hilo kwa kutumia busara zaidi.Tunatambua heshima yetu kwa nchi za Afrika Mashariki na kubwa zaidi tumekuwa wasuluhishi wazuri wa migogoro kwenye nchi za Afrika Mashariki.Hivyo busara itatumika kupata suluhu,”alisema Pinda na kuongeza “Serikali hatutapuuza haya yanayoendelea,”.


Mbowe katika maelezo yake bungeni alisema ana hofu na ushirikiano uliopo hasa baada ya Tanzania imeanza kutengwa na baadhi ya nchi za Jumuia ya Afrika Mashariki.

Alisema hatua ya nchi za Rwanda, Kenya na Uganda kuendesha vikao kupitia wakuu wa nchi ikiwemo kujitoa kwa nchi ya Rwanda kutumia Bandari ya Dar es Salaam, kunaashiria mwelekeo mbaya.

Rais Museveni ndiye Mwenyekiti wa Jumuia ya Afrika Mashariki, na ndio maana ameombwa na Tanzania kuwa msuluhishi wa mgogoro  kati ya Tanzania na Rwanda, unaoendelea chini kwa chini kati ya nchi mbili hizi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni